Sunday, October 21, 2012

SHEIKH FARID NA VIGOGO 4 KUPANDISHWA KIZIMBANI

Habari imeandikwa na Salma Said, Zanzibar -- VIGOGO watano wa Uamsho wanashikiliwa na polisi na wanatarajiwa kufikishwa mahakamani leo huku Jumuiya hiyo ikitoa waraka wa kuwataka Waislamu wadumishe amani.

Viongozi hao wako mikononi mwa polisi tangu juzi wakihojiwa mambo kadhaa likiwemo la kutoweka mmoja wao, Farid Had Ahmed ambaye ilidaiwa kuwa alikamatwa na polisi kwa siku nne.

Mbali na Farid, vigogo wengine wa Uamsho ambao wanahojiwa na polisi ni Amiri, Sheikh Mselem Ali Mselem (Naibu wake), Azzan Khalid Hamdan, Mussa Juma na Hassan Bakar.

Kamishna wa Polisi wa Zanzibar, Mussa Ali Mussa alisema jana kwamba wanawahoji msheikh hao na watawafikisha mahakamani leo iwapo wataona kuna mashitaka ya kujibu.

Katika hatua nyingine, Uamsho imetoa waraka kwenye misikiti ya Zanzibar wakiwataka Waislamu wawe watulivu na kuhudhuria kwa wingi mahakamani leo wakiwa na vitambulisho vya Mzanzibari Mkaazi.

Waraka huo uliosambazwa unasema hivi: “Kama hali ilivyo na mnavyosikia mnaombwa muwe watulivu na mufanye subra na leo (jana) hapo Msikiti wa Mbuyuni hapatakuwa na muhadhara si Adhuhuri wala Alasiri. Mnachoombwa na viongozi wenu muwe wavumilivu na watulivu hadi kesho (leo) mufike mahakamani bila ya fujo na muchukue kopi za vitabulisho vyenu vya Mzanzibari.  Jingine ni kuwa msikae vikundi na mkawapa askari sababu, tunasisitiza amani na utulivu na Waislamu ni wenye kutii amri za viongozi wao. Tunasisitiza amani na utulivu pia subra na dua kwa wingi. Ukipata taarifa hii mjulishe na mwenzio toa kopi na uwape wengine. Wabillah taufq.”

Waraka huo ambao ulikuwa unasambazwa katika misikiti jana haukutiwa saini na mtu yeyote wala haukutaja umetolewa na nani.

Wakili wa Uamsho, Salim Tawfik alisema jana kuwa wateja wake watafikishwa mahakamani leo lakini akalaumu kwamba Polisi wamewahoji bila ya yeye kuwepo.

“Mimi nilikwenda polisi nikakuta Mselem anahojiwa nikataka kuingia wakanizuia, wakasema wataniita lakini hawakufanya hivyo,” alidai wakili huyo.

Hali ya Zanzibar imetulia lakini ulinzi wa polisi na askari wa vikosi vya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar wameimarisha ulinzi katika maeneo mbalimbali ya mji huu wakiwa wanazunguka na silaha mikononi.

No comments:

Post a Comment