Wednesday, July 3, 2013

"SUGU AMESAFISHWA KWA KUMTUKANA WAZIRI MKUU. FIKIRIA TUSI HILO LINGETOKA KWA MLALA HOI "...MBWANA


KILA mtu anajua kuwa sheria na haki ni vitu viwili tofauti. Usilazimishe kupata haki, kwasababu sheria imeonyesha juu ya madai yako. Kufanya hivyo ni kujipotezea muda wako unaoweza kuutumia katika kazi nyingine za maendeleo yako.

Pamoja na  yote hayo, lakini wakati mwingine si sahihi kujificha kwenye mhimili wa kisheria kwa kufanya mambo ambayo ni tofauti katika jamii. Kila mmoja anapaswa kuishi kwa upendo bila kuweka u-mimi, vyama vyetu na mengineyo pia.


Nasema haya baada ya Mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi, maarufu kama ‘Sugu’kutoka (CHADEMA)kuachiwa huru na Mahakama ya Wilaya ya Mkoa wa Dodoma, kwa madai kuwa hati ya mashitaka ina mapungufu kisheria.


Sugu alipandishwa kizimbani katika mahakama hiyo, mbele ya Hakimu Mfawidhi wa Mkoa wa Dodoma, Elinaza Luvanda na kusomewa shitaka linalomkabili kuhusu kutoa lugha ya matusi katika mtandao wa kijamii, moja ya vitu vinavyotumiwa vibaya na watu wengi.

Katika mitandao hiyo, kila mmoja anaandika kile anachojisikia, bila kujali faida au hasara inayopatikana kwa kuandika upupu wake.


Sugu aliandika hivi;”Tanzania haijawahi kupata Waziri Mkuu mpumbavu kama Pinda”.

Kauli hii ilisababisha maswali mengi kwa Watanzania, hasa wakiamini kuwa imetokana na matamshi ya Waziri Mkuu Mizengo Pinda, kuwataka watu wapigwe watakapokaidi amri halali za jeshi la Polisi. Bila kuangalia sheria inasemaje juu ya sakata hilo, lakini kiubinadamu, Sugu hakupaswa kuandika maneno ya matusi dhidi ya Pinda.


Nasema hivi kwasababu Sugu kama mbunge wa Tanzania, alikuwa na nafasi kubwa ya kukataa agizo la mtu yoyote, kwa kutangaza bungeni. Angeweza hata kushawishi kutokuwa na imani na Pinda, kama wabunge wengi walivyowahi kufanya. Lakini Sugu alifanya haya kihuni tu. Akiamini kuwa mihemko ya kisiasa au sheria zitambeba.

Mambo kama haya yanasababisha kutokuelewana katika jamii. Leo hii kama sheria hazitamki wazi juu ya kosa hilo, basi yoyote anaweza kufanya anavyojisikia bila kuogopa chochote.


Je, mwingine ajitokeze mchana kweupe, kuandika au kusema kiongozi mfano wa Pinda ni mpumbavu? Je, serikali hii inaongozwa na wapumbavu? Je,Msajili wa Vyama vya siasa, John Tendwa naye ni mpumbavu?  Kiubinamu ukilizungumzia neno upumbavu, hasa kwa viongozi wetu ni jambo la kutia kichefu chefu.


Sugu angeyasema hayo kwa watu anaofanana nao, iwe kicheo au kiumri. Umri wa Sugu na Pinda haufanani kamwe. Hivyo kuusema upumbavu wa Pinda hadharani ni kumvunjia heshima kupita kiasi. Tuukatae hadharani.

Mtindo huu ukidhihiri hauwezi kudumisha utu na uungwana wetu. Siku zote uungwana ni vitendo.

Angalia, mwendesha mashitaka ambaye ni Wakili wa Serikali, Harieti Lopa  alidai mtuhumiwa alitenda kosa la kutoa lugha ya matusi kwa Waziri Mkuu, Pinda Juni 24, mwaka huu eneo la Manispaa ya Dodoma.


Alifika mbali zaidi kwa kudai mshitakiwa huyo, ambaye ni Sugu aliandika ujumbe huo bila kuutaja, ambao unaleta uvunjifu wa amani kwa Waziri Mkuu, hivyo ni kosa la jinai kwa mujibu wa Sheria kifungu kidogo namba 89 (a).


Sakata hili wakati linaendelea kuchambuliwa kwa mujibu wa sheria zetu, mshitakiwa alikana shitaka ndipo Wakili wa Serikali kuiomba mahakama itaje tarehe nyingine ya kutajwa kwa kesi hiyo.


Hata hivyo, Sugu alitetewa na mwanasheria wake, ambaye pia ni Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu, alikataa kesi hiyo kupangiwa siku nyingine, akisema hati ya mashitaka ni mbovu na haikukidhi matakwa ya sheria ya jinai.


Lissu anasema “Hati ya mashitaka,  inatuhumu kosa ni kutumia lugha ya matusi kifungu cha 89 (i) kifungu kidogo (a) katika Sheria zetu ambapo matusi yenyewe hayajatajwa, bali yanatolewa maelezo ya kosa kuwa lugha ya matusi ambayo inaweza kuvunja uvunjifu wa amani kwa Pinda, hiyo lugha ya matusi ni ipi,” Lissu alihoji.


Lissu alifika mbali zaidi kwa kusema kuwa upungufu mwingine wa kisheria ni hati ya mashitaka ipo kimya, hivyo kushangaa mshitakiwa atajitetea kwa lipi na ataandaa utetezi namna gani, wakati anachodaiwa kukiweka mtandaoni kikiwa hakijasemwa?

Maneno ya mwanasheria huyu yalipatiwa ufumbuzi na hakimu kujiridhisha kisheria na kukiri kuwa ni kweli  hati hiyo ina upungufu wa kisheria kwa mujibu wa kifugungu cha Sheria Namba 132 sura ya 20 na hivyo kuifutilia mbali  hati hiyo ya mashitaka ikiwa ni pamoja na kumuachia huru Mbunge huyo.

Pamoja na yote hayo, si malalamiko yangu kuachiwa kwa Sugu, ila namna watu watakavyoweza kutumia udhaifu huo kuwatendea wengine.

Kila mtu anaweza kufanya kama alivyotenda Sugu, dhidi ya mwingine. Nani anaweza kukamatwa leo akiandika kuwa Katibu Mkuu wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Willbroad Slaa ni mpumbavu kwasababu ameacha upadre na kuhamia kwenye siasa, tena Chadema?

Ni kutokana na hilo, nadhani kuna haja sasa wanasiasa wetu, akiwamo Sugu kuona kuwa siasa haziwezi kumfanya ajipachike uwendawazimu.

Lazima ajuwe kuwa heshima ni kitu ch abure, hivyo aihusudu ili afike mbali zaidi katika harakati zake.

Sina chuki dhidi ya wanasiasa hawa.Kila mtu anataka mabadiliko ya kisiasa na kiutawala, ila si kwa njia ya uvunjifu wa amani.

Kwa sasa wapo watu ambao hawataelewa uvunjifu wa amani utatokea wapi juu ya sakata la Sugu na Pinda.

Lakini Pinda kama Waziri Mkuu pia ni kiongozi kutoka Chama Cha Mapinduzi (CCM), chini ya Mwenyekiti wake Jakaya Mrisho Kikwete.

Ukiacha uongozi wake katika chama na serikali, anabaki kama binadamu wa kawaida mwenye ndugu au marafiki.


Hivyo basi, katika sakata hili, kuna siku baadhi yao watashindwa kukubali utu wa mtu unavyotolewa kwa ajili ya siasa za maji taka. Hao watagoma kusubiri. Watataka kulipiza kisasi, hivyo kuashiria kuwa usalama utakuwa kwenye mashaka makubwa. 

 Haya si ya kukubali yaendelee kufanyika katika Taifa hili linalokabiriwa na sekeseke la siasa.
Tusikubali kabisa, hivyo Sugu kama Mbunge alipaswa kujiheshimu na kuheshimu wengine, akiamini kuwa chochote atakachosema kitaonekana.


Mitandao ina nguvu kubwa mno. Watu wengi sasa wamekuwa humo. Ndio maana maandishi machache aliyosema, lakini yameibua mzozo hadi kufikishwa polisi.

Kuukosoa uamuzi wa mahakama juu ya kutukanwa kwa Pinda, hakuendi sambamba na kuwalimisha kumfikisha tena Sugu mahakamani, ila kumfanya ajuwe anapaswa kujichunga na anachokisema.
 
Hati ya mashtaka kama ina makosa, mapungufu, inaweza kuwekwa sawa, lakini hatua hiyo itaendeleza kujenga uhasama kati ya viongozi hawa.

Suala hili la Pinda juu ya amri yake kwa polisi ni tatizo, ila hakumfanyi atukanwe kama mtoto.
Ndio maana alipotoa tamko hilo wanaharakati walilipinga, ila si kwa njia ya kumvunjia heshima kama alivyofanya Mbunge Sugu.


Nadhani tunawajibu wa kuishi kwa upendo na kuheshimiana, ukizingatia kuwa kutaleta maendeleo ya kweli.

Tusitumie udhaaifu wa mapungufu kaatika sheria zetu kuwakandamiza wenzetu, maana leo kwa Pinda kesho Freeman Mbowe, Mwenyekiti wa Chadema na Mbunge wa Hai, Mwenyekiti wa Chama Cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Haluna Lipumba, Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana na viongozi wengine.
0712 053949
-Via Michuzi

No comments:

Post a Comment