
PICHA NA YUSSUF SIMAI-MAELEZO ZANZIBAR.

NA RAMADHANI ALI/ HABARI MAELEZO
Jamii imeshauriwa kuongeza juhudi katika kujilinda na kupambana na maambukizi ya virusi vinavyosababisha maradhi ya Ukimwi kwa vile maradhi hayo bado yapo na yanaendelea kupoteza maisha ya wananchi wengi nchini pamoja na kuonyesha dalili za kupungua.
Ushauri huo umetolewa na Waziri wa Afya Juma Duni Haji katika Maadhimisho ya siku ya Ukimwi Duniani zilizofanyika Skuli ya Msingi Mangapwani baada ya kuzindua Mkakati wa Awamu ya pili wa Uhamasishaji na Utetezi dhidi ya UKIMWI Zanzibar.
Amesema njia muafaka inayohitajika ni kwa kila mtu kufanya juhudi ya kujikinga asiambukizwe kwa kujizuia kujamiiana, kuwa mwaminifu katika ndoa na kutumia kinga kwa mtu anaehisi kunaulazima kufanya tendo la ndoa.
Waziri wa Afya amesema kuongezeka kwa maradhi ya Ukimwi kunarudisha nyuma mipango ya Serikali ya kuimarisha Uchumi na Ustawi wa Jamii kwani rasilimali chache zilizopo zitaelekezwa katika kupambana na maradhi hayo.
“Juhudi za kupambana na ukimwi zielekezwe kufikia wito wa mashirika ya kimataifa ya kuzifikia zero tatu, ambazo ni zero katika kuzuia maambukizi mapya, zero katika kupunguza unyanyapaa na zero katika kudhibiti vifo vinavyotokana na Ukimwi ifikapo mwaka 2016” alisema Waziri Dnni.
Amekemea tabia mbaya ya kuwanyanyapaa watu wanaoishi na virusi vya ukimwi na watoto ambao wazazi wao wamefariki kutokana na maradhi hayo kwani kufanya hivyo kunaathiri juhudi za kupambana na maradhi hayo.
No comments:
Post a Comment