Monday, January 7, 2013

RIPOTI YA KILICHOMUUA MWANAFUNZI HOTELI YA KITALII DAR KUTOLEWA


Ndugu wa aliyekuwa mwanafunzi wa kidato cha pili katika Shule ya Sekondari Juhudi, Gongo la Mboto, marehemu Jacqueline Matiko, wakitoka katika Hospitali ya Taifa Muhimbili jijini Dar es Salaam  mara baada ya uchunguzi wa mwili, uliofanyika juzi.
Kulingana na maelezo ya mmoja wa madaktari kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili walioufanyia uchunguzi wa kitabibu mwili wa marehemu Jacqueline Matiko, mwanafunzi wa kidato cha pili katika Shule ya Sekondari Juhudi iliyopo Gongo la mboto, amesema ripoti ya madaktari kuhusu uchunguzi wa sababu za  kifo hicho cha kutatanisha  itaiwasilishwa polisi kwa ajili ya hatua zaidi.
Mwanafunzi huyo  alikutwa amekufa maji  Januari Mosi mwaka huu katika Hoteli ya Southern Beach, iliyopo Kigamboni jijini Dar es Salaam.
Kamanda wa Polisi Temeke, Englebert Kiyondo, alikiri kukutwa kwa mwili wa mwanafunzi huyo na kwamba  kutokana na madai ya ndugu zake, mwili huo umefanyiwa uchunguzi katika Hospitali ya Taifa Muhimbili  na jeshi lake linasubiri ripoti ya madaktari.
Utata huo unatokana na ndugu wa marehemu ambao walikuwa nao siku ya tukio, kupingana na maelezo ya wafanyakazi wa hoteli hiyo kuwa marehemu alifia katika bwawa la kuogelea na inadaiwa siku ya tukio marehemu alipotea katika mzingira ya kutatanisha akiwa hotelini hapo,  mpaka waliporudi kesho yake nakukuta mwili wake umefunikwa kwa shuka, pembeni ya bwawa la kuogelea.
“Inashangaza wenzangu walikuja wakaambiwa hajaonekana lakini tuliporudi tena baadaye, bila kutarajiwa tukaukuta mwili. huku askari polisi wakiwa wameitwa kuja kuuchukua,”Musa Matiko.
Baadhi ya kinamama ambao walishiriki katika kuosha mwili wa marehemu mwanafunzi huyo waliliambia Mwananchi kuwa kuna kila dalili kuwa binti alibakwa kisha kunyongwa kwani shingo yake ilikuwa imevimba na pia alikuwa na michubuko sehemu za siri.
“Amebakwa kisha akanyongwa hilo halina ubishi ila tusubiri ripoti za daktari,” alidai bibi wa mtoto huyo, Saida wakati anatoka katika chumba cha kuhifadhi maiti katika Hospitali ya Muhimbili baada ya kuosha mwili wa marehemu, ambaye alizikwa katika makaburi ya Gongolamboto, mwishoni mwa wiki iliyopita.
Chanzo Mo Blog

No comments:

Post a Comment